Wednesday, May 16, 2012

Shule ya msingi Pambalu

ELIMU

Pambalu shule inayoongoza katika kufaulisha Wanafunzi katika Wilaya ya Sengerema.

LICHA ya ubora wao huo, wazazi hufurahi, watoto wao wanapopata mimba kwa lengo la kuwaoza ili wapate fedha MARA nyingi shule zilizoko mijini ndizo zinazofaulisha zaidi wanafunzi kwa ajili ya kuendeleza masomo katika elimu ya sekondari mara baada ya kumaliza elimu ya msingi. 
Katika picha ni baadhi ya wanafunzi wakiwa katika mapumziko
Wananchi wengi wamekuwa wakisikika na hata kusema kuwa wanafunzi wa vijijini hawawezi kufaulu kutokana na mazingira yenyewe kuwa duni mno katika masomo yao.

Na kuna baadhi husikika wakisema kuwa wanafunzi wa kijijini ndiyo wana akili zaidi kuliko wa mjini na pale wanaposhindwa kuchaguliwa kwa ajili ya kuendelea na masoma ya Sekondari wanasema kuwa rushwa ndiyo inayo changia watoto wakijijini kuachwa. Wanasema kuwa wanafunzi wengi wa mijini baba zao wanakuwa na uwezo hivyo hata kama mtoto akifeli basi jina la mtoto wa kijijini linakatwa na linaingizwa jina la mtoto wa mjini.

Na dhana hiyo imekuwa ikiwaingia wazazi wengi wa vijijini na kuona kuwa watoto wao wanaonewa katika uchaguzi wa wanafunzi wa kuendelea na masomo. Lakini kwa upande mmoja au mwingine dhana hiyo inaweza kuwa ni ya kweli au ni kasumba tu iliyojengeka miongoni mwa jamii ya vijijini.

Shule ya Pambalu iliyoko katika Wilaya hii ya Sengerema katika Mkoa wa Mwanza ni moja ya shule iliyoko katika mazingira duni sana ya utoaji wa elimu kwa wanafunzi washuleni hapo.

Licha ya kuwa na mazingira duni na kuwa kijijini lakini matokeo ya shule hiyo yamekuwa ya kushangaza kama si ya kufurahisha kwani moja ya shule katika Wilaya ya Sengerema inayotoa wanafunzi wengi zaidi kwa ajili ya kujiunga na masomo ya Sekondari.

Mwalimu Mkuu Msaidizi wa Shule hiyo, Malale Mathias anaielezea hali hiyo kama alivyozungumza na mwandishi wa makala hii katika shule hiyo. Anasema kuwa siri kubwa ya shule hiyo kufaulisha sana wanafunzi ni kutokana na walimu wa shule hiyo walivyo kuwa na mikakati ya kukuza elimu katika Wilaya yao na ushirikiano mkubwa baina ya walimu. Anasema kuwa licha ya walimu wa shule hiyo kuwa na ushirikiano na wanafunzi wao pia wanafunzi wenyewe wamekuwa na mwamko wa elimu hiyo hali inayopelekea wanafunzi hao kufanya vizuri katika kila mtihani. Akizungumzia twakwimu ya shule hiyo kwa kipindi cha mwaka wa 1999 hadi 2001 anasema kuwa jumla ya wanafunzi 240 walichaguliwa kuendelea na masoma ya Sekondari.

Anasema kuwa katika wanafunzi hao Wasichana walikuwa 130 na Wanaume walikuwa 110 na kufanya idadi ya wanafunzi hao kuwa 240 kwa kipindi hicho cha miaka mitatu.

Akizungumzia idadi kubwa ya wasichana katika kufaulu anasema kuwa inatokana na wasichana kupewa kipaumbele katika maksi hivyo wanaume inawalazimu kufanya kazi ya ziada ili kuchaguliwa kutokana na ukweli kuwa maksi zao ni za juu zaidi kulinganisha na wasichana. 
Mandhari ya nje katika shule ya msingi Pambalu kama inavyoonekana kwenye picha hapo juu
Anasema licha ya kuwa na matokea mazuri katika shule hiyo pia kuna tatizo la vyumba vya madarasa kuwa vichache na hivyo kulazimika watoto wengine kukaa chini wakati wa vipindi kama alivyoshuhudi mwandishi.

Licha ya tatizo hilo pia anasema kuwa kuna baadhi ya wazazi wa watoto wanaosoma katika shule hiyo kuwa na tabia ya kufurahia pindi watoto wao wa kike wanapopata ujauzito kwa lengo la kuwaozesha na kupata fedha.

"Tatizo hili kwa shuleni kwetu limekuwa sugu sana kwani kuna baadhi ya wazazi wamekuwa wakifurahia watoto wao kupata ujauzito na kuwaoza ili wapate fedha za matumizi," anasema mwalimu huyo.

Akizungumzia historia ya shule hiyo mwalimu Malale anasema kuwa jina la shule hiyo limetokana na mzee mmoja aliyekuwa akiishi katika eneo hilo la shule, alikuwa akifahamika kwa jila hilo la PAMBALU.

Anasema kuwa shule hiyo ilianzishwa rasmi mnamo Novemba 11 mwaka 1971 chini ya mwalimu Mkuu wa kwanza Silivester Likonge.

"Toka kuanzishwa kwa shule hii kume kuwa na walimu wapatao 13 waliongoza shule hiyo mpaka sasa,"anasema mwalimu huyo.


Historia ya Wilaya ya Sengerema.

HISTORIA

WILAYA ya Sengerema ni moja ya Wilaya nane zilizounda Mkoa wa Mwanza . Wilaya hii ilizinduliwa rasmi mwaka 1975 baada ya kumegwa kutoka katika wilaya ya Geita.

Wilaya ya Sengerema kwa upande wa kaskazini imepakana na Wilaya ya Ukerewe, kwa upande wa mashariki imepakana na Wilaya ya Nyamagana na Iemela, kwa upande wa magharibi imepakana na Wilaya ya Geita, Kusini imepakana na Wilaya ya Misungwi na Geita.

Wilaya inaeneo la ukubwa wa kilometa za mraba 8,817 kati ya hizo kilometa za mraba 3,335 ni eneo la nchi kavuna kilometa za mraba 5,482 ni eneo la maji ya Ziwa Victoria.Kati ya eneo la nchi kavu kilometa za mraba 2,511 sawa na 75% ni ardhi yenye rutuba inayofaa kwa kilimo na Ufugaji wakati ambapo kilometa za mraba 824 sawa na asilimia 25% ni eneo la misitu ya asili, hifadhi na majabali.  Ni moja ya Wilaya changa nchini chimbuko ni vijiji vinne

KWA ujumla utakapouliza chimbuko la kijiji, Tarafa, Wilaya, Mkoa na hata Nchi fulani utaambiwa kuwa chimbuko la jina la kijiji hicho au Wilaya na hata nchi hiyo ni jina la mtu mmoja ambaye mara nyingi anakuwa tayari ni marehemu, ambaye alikuwa maarufu sana hapo zamani au jina la sehemu hiyo linaweza kuwa ni kutokana na maafa yaliyowahi kuikumba sehemu hiyo.

Hiyo ndiyo hali halisi ya matokeo ya nchi, mkoa, wilaya, tarafa na vijiji, mara nyingi majina hayo yanakuwa ni ishara ya kumkumbuka ya mtu huyo au maafa hayo na mara nyingi inakuwa kama sehemu ya historia kwa watoto wanaozaliwa na kwa watalii katika mkoa huo au nchi hiyo.Mfano mzuri wa mambo hayo ni Wilaya moja

inayojulikana kama Songea, chimbuko halisi la jina la Wilaya hiyo inatokana na Chifu wa kwanza katika Wilaya hiyo katika miaka ya zamani na hadi kuja jina lake kutukuzwa hadi leo hii ni kutokana na ushujaa wake wa kupinga utawala wa mkoloni ambaye alikuwa ni Mjerumani.
Mpaka leo hii ukienda katika Wilaya hiyo ya Songea utapakuta mahali aliponyongewa chifu huyo kwani pametengenezwa na kusafishwa vizuri na kazi hiyo hufanywa na Halmashauri ya Wilaya hiyo pamoja na zana iliyotumika kwa ajili ya kumnyongea chifu huyo na ile ndoano ailiyomyonga kwa kuning’inizwa katika mti mmoja iliopo mpaka leo na mti huo unaheshimika sana pale Songea.

Mji wa Sengerema kama unavyoonekana katika picha Tukirudi katika Wilaya ya Sengerema chimbuko lake ni tofauti kidogo kama ilivyozeleka kuwa ni urithi wa jina la mtu au ni kutokana na maafa yaliyowahi kutokea kwani chimbuko rasmi la Wilaya hii ni Vijiji vinne ambavyo ni Ibisabageni, Nyampulukano, Nyatukara na Mwabaluhi.
Kwa mujibu wa Afisa Ardhi wa Wilaya hii, Athuman Juma pamoja na baadhi ya wazee wa Sengerema ambao hawakuwa tayari kuyaweka majina yao peupe walipozungumza na mwandishi wa makala hii wanasema kuwa chimbuko la Wilaya hii ni kutokana na vijiji hivyo.

Afisa Ardhi huyo anasema kuwa kwa yeye ndiye mpimaji wa viwanja kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za wakazi wa Wilaya hii ameweza kupata chimbuko halisi la Wilaya hii na jinsi ilivyoanza hadi kuwa Wilaya katika miaka ya 70.

Anasema kuwa katika kipindi hicho cha miaka ya nyuma sehemu za Ibisabageni zilikuwa ni pamoja na maeneo yote ya kuanzia kwenye bwawa la Sengerema na kuelekea katika njia ya Busisi, Sekondari ya Sengerema, Seminnary ya Saint kalori na maeneo ya kusini mwa Mji wa Sengerema pamoja na maeneo yote ya kusini Mashariki mwa Wilaya hii kwa sasa, yote hayo yalikuwa chini ya kijiji cha Isibageni.

Nao wazee hao wanasema kuwa kijiji cha Nyampulukano kilichukua maeneo yote ya mji yaliyobakia, misheni, shule ya Nyampulukano, Sengerema Seminary pamoja na maeneo ya kiwanja cha mnada wa ng’ombe kwa hivi sasa.

Wanasema kuwa kijiji cha Mwabaluhi kilichukua maeneo yote ya Bomani na kuendelea hadi katika maeneo ya kata ya Igalula na kuendelea.Nacho kijiji cha Nyatukara kilichukua maeneo yote ambayo yako mbele ya misheni hadi katika vijiji jirani ambavyo kwa sasa vinajitegemea kuelekea Kamanga kwa mujibu wa wazee hao.

Afisa Ardhi anasema kuwa licha ya mwaka 1985 vijiji vyote hivyo vimeungana na kuwa Wilaya ya Sengerema lakini bado vijiji hivyo vinatumia taratibu za vijiji vyao kwani bado vina mtendaji wa mtaa kama ilivyo kwa vijijini.

Licha ya hilo anasema kuwa tangu ahamie na alivyokuwa anaisikia Wilaya ya Sengerema hajawahi kusikia Wilaya hii ikiwa katika ukosefu wa chakula kwani ina ardhi kubwa na yenye rutuba ambayo hata kama wakazi wote wa Wilaya hii wakagawana sehemu zao ardhi itakuwa imebaki bado kubwa tu.

Anasema kuwa uchumi mkubwa wa Wilaya hii unategemea sana kilimo na uvuvi kutokana na kuzungukwa kwa kiasi kikubwa na ziwa Vicktoria na hivyo wakazi wengi kujikita katika uvuvi.

Kwa mujibu wa wazee wa Wilaya hii wanasema kuwa mji wa Sengerema unapanuka kwa kiasi kikubwa sana na hivyo wanauhakika baada ya miaka mitano Sengerema haitakuwa kama ilivyo sasa kwani itakuwa imeendelea kwa kiasi kikubwa sana ukilinganisha na baadhi ya Wilaya nyingine katika Mkoa wa Mwanza.

Hata hivyo wazee hao wanasema kuwa Wilaya hii haina wakazi wengi sana ambao ni wasukuma kwani wamechanganyika na wakerewe ambao walikosa ardhi katika kisiwa chao na hivyo kuhamia katika Wilaya ya Sengerema, hata hivyo wanasema kuwa licha ya kuwa na wakerewe lakini hakuna mtu anayeweza kutambua hilo kwani kiluga cha kikerewe ni sawa tu na kisukuma kwani wanasikilizana vizuri tu.

“Wasukuma wengi wapo katika kijiji cha Mwabaluhi na Nyachenche na ndiyo wafugaji wakubwa wa ng’ombe ukilinganisha na vijiji vingine vya Sengerema,” wanasema wazee hao.

Hata hivyo Afisa Ardhi anasema kuwa Wilaya hiyo itapanuka kwa kiasi kikubwa kutokana na watu wengi ambao wameshapimiwa sehemu zao za kujenga kutojenga na mara watakapoanza ujenzi wa sehemu zao basi mji huu utapanuka sana.

“Tumepima viwanja Elfu kumi (10,000) kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za kisasa lakini mpaka sasa nyumba zilizojengwa ni elfu nne tu (4,000) hivyo naamini kuwa mara watu watakapo anza kujenga katika viwanja vyao basi mji utapanuka sana tena kwa haraka,” anasema Afisa Ardhi huyo wa Wilaya.

Wilaya ina jimla ya visiwa 39, visiwa 27 vinakaliwa na watu na visiwa 11 ni hifadhi na kambi za uvuvi.

<< Rudi Juu >>

Sunday, January 29, 2012

SAMAHANI SANA WADAU....

ndugu zangu kwa mda mrefu nimekuwa siweki updates katika  blog yangu hii inatokana na bize kidogo ya Semister exams.  naahidi kuanzia tarehe 6/2/2012  tutakuwa tukichambua habari muhimu za maendeleo ya elimu ktk wilaya yetu. tarehe 5/2/2012 kutakuwa na maboresho ya blog yetu, tutegemee mambo mazuri.......
wenu
              EMILIAN BARONGO
                elimukwetu manager.


Sunday, January 1, 2012

Nilivyopania kuinua kiwango cha Elimu Sengerema.


Ndugu zangu nikiwa kama mkazi na mwanafunzi niliyesoma kuanzia chekechea mpaka kidato cha nne katika wilaya ya Sengerema nimepania kunyanyua kiwango cha elimu katika wilaya yangu kwa kutoa huduma za kielimu kwa bei nafuu......nitazielezea hapo baade huduma ninazozito. Naomba wakazi wa Sengerema na Mwanza kwa ujumla wenu mniunge mkono.

Elimu Sengerema

ndugu zangu kiwango cha elimu katika wilaya yetu ya Sengerema kinazidi kuzorota, wakazi tunahitaji kuwekeza nguvu nyingi atika kuinua kiwango cha elimu wilayani Sengerema na mkoani Mwanza kwa Ujumla. hayo niliyagundua tarehe 23/09/2011 nilipohuzuria mahafali ya kidato cha nne katika shule ya sengerema sekondari moja ya shule zenye historia kubwa nchini Tanzania